Ni hapa...

Umefika mahali unapopahitaji ...karibu!

Posted by BM. on Monday, December 13, 2010

Mwanamuziki Dr.Remmy Ongara amefariki dunia alfajiri ya kuamkia leo nyumbani kwake Sinza jijini Dar .Katika siku za karibuni alilazwa hospitalini akisumbuliwa na ugonjwa wa kiharusi. Tayari mwili wa marehemu Remmy Ongara umeshapelekwa hospitali ya Muhimbili kuhifadhiwa ukisubiri taratibu za mazishi. Mungu aiweke roho ya Marehemu ongara peponi …amin.
Hebu tuangalie historia yake kwa kifupi yamwanamuziki huyu ambaye alijitengenezea umaaufu mkubwa katika uhai wake.

Ramadhani Mtoro Ongala alizaliwa mwaka 1947 Jamuhuri ya kidemokrasi ya kongo ?DRC eeo la kivu kaskazini, wakati huo ikijulikana kama Kongo Zaire. Baada ya kuzaliwa familia yake ilihamia Kisangani. Mzee Mtoro Ongara , baba yake Remmy alikuwa mpiga ngoma na mwimbaji na pia alikuwaakipenda sana kucheza mpira.
Ipo habari kwamba kabla ya kuzaliwa kwake mama yake alipata ujauzito mara mbili lakini kwa bahati mbaya kila mara mtoto alifariki. Alipopata ujauzito mara ya tatu alienda kwa mganga wa kienyeji kumuomba ushauri afanye nini ili mtoto atakayezaliwa asiiage dunia pia. Bila kusita mganga wa kienyeji akampa ushauri wake. Akamwambia kwanza asiende kujifungulia hospitali bali akajifungulie maporini. Pia alipewa ushauri kwamba mtoto akishazaliwa asije akamkata nywele zake. Yote hayo yalitendeka na ndio kisa cha Remmy Ongala kutokata nywele zake kwa muda mrefu sana.

Kwa bahati mbaya baba yake huyo alifariki dunia na kumuacha Remmy akiwa na miaka sita tu akiwa tayari ameshaanza shule. Lakini kutokana na ukosefu wa fedha na kwa sababu mama yake hakuweza kuendelea kumlipia shule, Remmy ilibidi aache shule.
Ilipofika miaka ya 60, Remmy tayari alikuwa ameshajifunza mwenyewe kupiga gitaa. Mwaka 1964 ulikuwa sio mwaka mzuri kwa Remmy kwani mama yake mzazi alifariki dunia jambo ambalo lilimuacha Remmy na mzigo wa kuwalea wadogo zake kwani yeye sasa ndio alikuwa mkuu wa familia.
Mwaka 1978 Remmy aliingia jijini Dar-es-salaam baada ya kuitwa na mjomba wake ili aje ajiunge na bendi maarufu ya wakati huo,Orchestra Makassy, iliyokuwa chini ya uongozi wa mjomba wake huyo, Mzee Makassy. Huo ndio ukawa mwanzo wa maisha ya Remmy nchini Tanzania. Akiwa na bendi ya Orchestra Makassy, aliandika wimbo wake wa kwanza uliojulikana kama “Siku ya Kufa”, wimbo ambao aliuandika kumkumbuka rafiki yake aliyefariki. Wimbo huo ulianza kumpatia umaarufu.


Alidumu na bendi ya Ochestra Makassy kwa kama miaka mitatu hivi kabla ya mwaka 1981 kuhamia katika bendi ya Orchestre Super Matimila iliyokuwa ndio inaanza kuchipukia miaka hiyo. Hiyo ilifuatia Mzee Makassy kuhamishia bendi yake nchini Kenya. Jina la bendi hiyo, Matimila, lilitokana na jina la kijiji kimoja kilichoko kusini mwa Tanzania. Baada ya kujiunga kwa Remmy, bendi ya Matimila ilijiongezea umaarufu katika anga za muziki nchini Tanzania wakati huo.
Miaka iliyofuatia ilishuhudia umaarufu wa Remmy ukiongezeka hususani kutokana na mashairi ya nyimbo zake ambayo yaliegemea katika kuzungumzia mambo halisi ya kijamii kama vile umasikini, siasa nk.
Pamoja na yote hayo, miaka michache iliyopita Dr.Remmy Ongala aliamua kuachana na muziki wa dansi kwa madai ya kwamba umejaa mambo mengi ya kishetani. Remmy akaokoka, akatubudu dhambi zake na hivi sasa anamuimbia bwana. Mapema mwaka huu alikuwa mbioni kukamilisha albamu yake ya pili. Bado anaishi Sinza (Kwa Remmy) mahali ambapo panaitwa hivyo kwa heshima yake.(Habari kwa msaada wa mitandao mbalimbali)

0 comments: